Rais wa Iran Hassan Rouhani amesema Marekani imeshindwa katika juhudi zake za kuiwekea tena vikwazo nchi hiyo baada ya washirika wake wa Ulaya kusema hatua hiyo haiambatani na msingi wa kisheria.
Katika hotuba iliyorushwa kupitia televisheni, Rais Rouhani alisema Iran "itajibu vikali uonevu wa Marekani dhidi ya nchi yake.
Utawala wa Marekani umesema vikwazo hivyo vinarejelewa tena chini ya mkataba wa nyuklia ambao Marekani ilijiondoa, huku Uingereza, Ufaransa na Ujerumani zikisema kuwa hazina uwezo wa kutekeleza hatua kama hiyo .
Nchi hizo tatu - pamoja na China, Urusi na Marekani zilitia saini mkataba 2015 kudhibiti mpango wa nyuklia wa Iran, Lakini utiaji saini huo ulianza kuwa na vuta n’kuvute baada ya Rais Donald Trump kuingia madarakani.
Kutokana na hilo, Iran ilianza kukiuka baadhi ya ahadi ilizotoa ikiwa ni pamoja na urutubishaji wa madini ya uranium zaidi ya kiwango kilichowekwa.
Marekani ilisema nchi hiyo inastahili kuchukuliwa hatua, na kutangaza kuwa vikwazo vyote vya Umoja wa Mataifa ambavyo vilikuwa vimesitishwa virudishwe tena - hatua ambayo ilikuwa imegonga mwamba.
Siku ya Jumamosi, Afisa wa ngazi ya juu wa Marekani ambaye jina lake halikutajwa aliiambia shirika la habari la Reuters kwamba kuanzia Jumatatu, Washington huenda ikaanza kuwawekea vikwazo baadhi ya watu na mashirika yatakayojihusisha na zana za nyukilia za Iran, makombora na mpango wake wa uundaji silaha ndogondogo.