Jeshi la Nchini Mali limeendelea kugonga vichwa vya habari ulimwenguni baada ya kufikia maamuzi ya kuteua viongozi katika nyadhifa mbalimbali leo Septemba 02,2020.
Kamati ya Kitaifa ya Wokovu wa Wananchi (CNSP), chombo kilichoundwa na kundi la jeshi lililofanya mapinduzi nchini Mali, Agosti 18, kinaendelea kujidhatiti. Viongozi kadhaa wameteuliwa kwenye nyadhifa mbalimbali wakati rais aliye kuwa Ibrahim Boubacar Keïta akilazwa hospitalini.
Miongoni mwa watu walioteuliwa na Jeshi hilo kuwa viongozi ni Cheick Oumar Traoré ameteuliwa kuwa mshauri maalum wa kiongozi wa mapinduzi, anayehusika na habari na mawasiliano.
Daktari Youssouf Coulibaly, ni raia mwingine aliyeteuliwa, kwenye nafasi ya mshauri maalum wa kiongozi wa mapinduzi, anayehusika na maswala ya kisheria.
Kwa upande wa Jeshi, Jenerali Souleymane Doucouré, ambaye alikuwa kiongozi wa zamani wa Msemaji wa sasa wa kundi la jeshi lililofanya mapinduzi ameteuliwa kuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Ulinzi, huku Jenerali Oumar Diarra ameteuliwa kuwa Mkuu mpya wa Jeshi la Mali.
Kundi hilo la wanajeshi waliofanya mapinduzi pia lilifanya mabadiliko mengine kwenye nafasi muhimu jeshini na kwenye idara ya ujasusi.
Wakati huohuo aliyekuwa Rais wa Mali Ibrahim Boubacar Keita (IBK) amelazwa hospitalini tangu Jumanne ya wiki hii katika hospitali moja mjini Bamako.
Hata hivyo mmoja kati ya wasaidizi wake amesema kuwa Bwana Keita amekwenda kufanya vipimo vya kawaida vya afya yake hospitali.
Mwanasiasa huyo wa miaka 75 alizuiliwa kwa siku kumi na wanajeshi kabla hajatangaza kujiuzulu na baaadaye ndipo aliachiliwa huru.
Aidha, kwa miezi kadhaa upinzani ulikuwa ukimshinikiza kujiuzulu na kumlaumu kwa kurudisha nyuma uchumi wa nchi, kudhibiti ufisadi na kushindwa kukabiliana na makundi ya kijihadi.