Maalfu ya watu wameshiriki katika maandamano makubwa kabisa, kuwahi kufanyika hadi sasa nchini Sudan ya kumtaka Rais wa nchi hiyo Omar al-Bashir ang’atuke baada ya kutawala kwa muda wa takriban miaka 30.
Waandamanaji walikwenda hadi kwenye makao makuu ya jeshi mjini Khartoum, huku wakipaza sauti zao wakisema, amani, haki na uhuru. Makaazi ya rais al-Bashir pia yamo kwenye makao makuu hayo. Waandaaji wamesema kabla ya maandamano hayo kuanza idadi kubwa ya polisi waliwekwa katika sehemu mbalimbali za mji mkuu, Khartoum ambapo waliwazuia wapita njia kuzifikia sehemu kadhaa za mji huo. Kwa mujibu wa taarifa maandamano hayo yalifanyika kwa usalama. Tangu kuanza harakati za wananchi, mnamo mwezi Desemba za kumtaka rais al-Bashir aachie ngazi, watu 31 wameshauawa. Shirika la kutetea haki za binadamu la Human Rights Watche limesema linaamini kwamba watu 51 waliuawa wakiwemo watoto na wahudumu wa afya.
CHANZO: Idhaa ya Kiswahili DW