Serikali ya Msumbiji imesema visa vilivyothibitishwa vya maambukizi ya ugonjwa wa kipindupindu katika mji wa Beira vimeongezeka maradufu na kufikia wagonjwa 271 katika kipindi cha masaa 24 yaliyopita.
Serikali na wafanyakazi wa mashirika ya kutoa misaada wanajaribu kudhibiti kusambaa kwa maradhi hayo wiki mbili tangu kimbunga Idai kilipoupiga mji wa Beira na kusababisha mafuriko makubwa yaliyowauwa zaidi ya watu 700 katika nchi za Msumbiji, Zimbabwe na Malawi.
Akizungumza wakati wa kufungua kituo cha muda cha matibabu ya kipindupindu mjini Beira, waziri wa Mazingira wa Msumbiji amesema tayari wagonjwa 138 wanapatiwa matibabu na kwamba hadi sasa hakuna aliyefariki dunia kutokana na maradhi hayo kwenye hospitali zinazotoa huduma.
Maeneo mengi nchini Msumbiji na Zimbabwe ambayo yalipigwa vibaya na kimbunga Idai bado hayafikiki kwa njia ya Barabara. Maradhi ya kipindupindu ni tatizo sugu nchini Msumbiji ambayo imeshuhudia miripuko ya mara kwa mara katika miaka mitano iliyopita na kulingana na shirika la Afya duniani kiasi watu 2000 walipatwa na kipindupindu wakati mlipuko wa mwaka 2018.
CHANZO: Idhaa ya Kiswahili DW