Waandamanaji katika mji wa Goma mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo wameshambulia na kuharibu kambi ya vikosi vya Umoja wa Mataifa kushinika ziondoke nchini humo.
Monusco inalaumiwa kwa kushindwa kuleta amani mashariki mwa DRC kwa zaidi ya miaka 20 tangu vikosi hivyo kupelekwa katika eneo hilo linalokumbwa na ghasia.
Picha zilizoshirikishwa katika mitandao ya kijamii zinaonyesha watu wakiimba kupinga uwepo wa vikosi vya kulinda amani nchini DRC, wengine wakiondoa nyenzo za msingi wa kituo chao kikuu huko Goma.
Masoko na maduka mengi yamefungwa Jumatatu katika mji unaokaribia watu milioni moja kwa hofu ya kuzuiwa na waandamanaji, Eliezer Makambo mfanyabiashara wa ndani aliiambia BBC Maziwa Makuu.
Msemaji wa serikali, Patrick Muyaya, amesema kwenye Twitter kwamba serikali "inalaani aina yoyote ya mashambulizi dhidi ya wafanyakazi wa Umoja wa Mataifa na majengo".
Muyaya ameongeza kwa kubainisha waliohusika na maandamano ya Jumatatu mjini Goma "wataadhibiwa vikali".