Mkuu wa Umoja wa Afrika, Rais Macky Sall wa Senegal, ameeleza "wasiwasi mkubwa" kutokana na kuongezeka kwa mvutano kati ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo na Rwanda.
Rais Sall amebainisha kwamba kila nchi inaishutumu nyingine kwa kuunga mkono makundi ya waasi yenye silaha ambapo ameomba kuwepo na utulivu na kuzitaka pande zote mbili kutatua mzozo wao kupitia mazungumzo.
Siku ya Jumamosi Rwanda ilisema wanajeshi wake wawili Élysée Nkundabagenzi na Ntwari Gad walikuwa wakishikiliwa mateka mashariki mwa DR Congo na wanamgambo wa Kihutu wa Rwanda wa FDLR, ambayo inasema inapata uungwaji mkono kutoka Kinshasa.
Hapo awali, DR Congo ilisitisha safari za ndege kuelekea Rwanda na kumwita balozi wa Kigali ikimtuhumu jirani yake kuwaunga mkono waasi wa M23, ambao sasa inawataja rasmi kuwa magaidi.
Kundi la M23 pia limetengwa katika mazungumzo ya amani ya Nairobi kati ya serikali ya Congo na makundi mengi ya wanamgambo wanaopigana katika eneo lake la mashariki.
#ChanzoBBC