Mataifa ya Afrika Magharibi yamekubaliana kuiwekea Mali vikwazo vikali ikiwemo kufunga mipaka yao, kuvunja mahusiano ya kidiplomasia na kuweka vikwazo vikali vya kiuchumi.
Vikwazo hivyo vipya kutoka Jumuiya ya Kiuchumi ya Mataifa ya Afrika Magharibi – ECOWAS yenye nchi 15 wanachama vinaonyesha jinsi ilivyoufanya msimamo wake kuwa mgumu kuelekea Mali, ambayo viongozi wa mpito wamependekeza kuandaa uchaguzi Desemba 2025 badala ya Februari mwaka huu kama walivyokuwa wamekubaliana awali.
Katika taarifa ya pamoja baada ya mkutano wao wa dharura mjini Accra, Ghana, ECOWAS imesema hatua ya serikali ya kijeshi kuchelewesha utaratibu wa kurejesha utawala wa kiraia haikubaliki kamwe.
Jean-Claude Kassi Brou ni Rais wa Halmashauri Kuu ya ECOWAS "Hii ina maana kuwa serikali haramu ya mpito ya kijeshi itawashikilia mateka watu wa Mali kwa miaka mitano ijayo.
Jumuiya hii inasisitiza wito wake kwa viongozi wa mpito kuzingatia shughuli zinazolenga kurejea kwa haraka kwa utaratibu wa kikatiba."
Jumuiya hiyo imesema imekubaliana kuweka mara moja vikwazo vipya vya ziada. Ni pamoja na kufungwa mipaka ya ardhini na angani ya wanachama wake na Mali, kusitishwa kwa miamala isiyo ya lazima ya kifedha, kufungia mali za serikali ya Mali katika benki za kibiashara za ECOWAS na kuwaita mabalozi wao kutoka Bamako.