Marudio ya kura za urais nchini Kenya yanaendelea. Katika maeneo mengi Kisumu, mji ambao ni ngome ya Raila Odinga, wakazi wamefunga barabara na kuchoma matairi wakipinga marudio ya kura za urais. Kinara wa upinzani NASA alikuwa amewahimiza wafuasi wake kutoshiriki kwenye kura za leo.
Polisi nchini humo wasema raia mmoja aliyepigwa risasi na polisi katika maandamano yenye vurugu amefariki dunia akiwa hospitali. Tukio hilo limetokea Kisumu na imeripotiwa kuwa vijana wengine watu waejeruhiwa na risai na wapo hospitalini.
Licha ya haya, kura zimeendelea kwenye maeneo mengine ila idadi ya wapiga kura imekuwa ndogo sana ikilinganishwa na uchaguzi uliopita. Rais Uhuru Kenyatta wa chama cha Jubilee amepiga kura yake katika eneo la Mutomo, Gatundu katika kaundi ya Kiambu.
Amesema amefurahia kwamba raia wanajitokeza kupiga kura. "Tumechoshwa na uchaguzi na sasa ni wakati wa kusonga mbele. Uchaguzi ni fursa kwa raia kuwachagua viongozi kama ilivyosema Mahakama ya Juu. Hebu tuwachague viongozi na tusonge mbele," amesema.
Kwa Hisani ya BBC Swahili