Wasafiri kutoka Dubai wataruhusiwa kuingia nchini Kenya kuanzia leo baada ya nchi hiyo kuondoa marufuku iliyokuwa imeweka kwa ndege zote zinazoingia na za abiria kutoka taifa hilo la Mashariki ya Kati wiki mbili zilizopita.
Mkurugenzi mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga nchini Kenya (KCAA) Gilbert Kibe ameliambia gazeti la Business Daily kwamba marufuku hiyo iliondolewa Jumatatu usiku wa manane, na kutoa afueni kubwa kwa mamia ya wasafiri kati ya maeneo hayo mawili.
Kenya ilikuwa imesimamisha safari zote za ndege za abiria zinazoingia na kutoka Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) mnamo Januari 10 kulipiza kisasi dhidi ya hatua ya Dubai kupiga marufuku safari zote za ndege za abiria kutoka Kenya kwa madai ya vipimo bandia vya Covid-19.
Marufuku hiyo hata hivyo haikuathiri safari za ndege za mizigo ambazo kwa kawaida husafirishwa na wachukuzi kama vile Kenya Airways (KQ) na shirika la ndege la Emirates kutoka UEA hadi Kenya.
"Kenya itafanya NOTAM kuondoa kusimamishwa kwa safari za ndege kwenda na kutoka UAE kuanzia usiku wa manane leo (Jumatatu)''-alisema Bw Kibe.
Marufuku hiyo ilikuja siku chache baada ya UAE kuongeza muda wa marufuku ya safari za ndege nchini Kenya baada ya kubaini kuwa wasafiri kutoka Nairobi walipimwa na kukutwa na Covid-19 baada ya kuwasili katika taifa hilo la Mashariki ya Kati, licha ya nyaraka zao kuonesha hawana maambukizi.