Mahakama ya Rwanda hii leo imeaanza kusikiliza kesi dhidi ya Paul Rusesabagina na wengine 20 ambao wanakabiliwa na mashtaka ya ugaidi.
Rusesabagina, ambaye amekuwa mkosoaji wa Rais Paul Kagame, anatuhumiwa kuunga mkono shughuli za kikosi cha National Liberation (FLN), ambacho ni mrengo wa wanamgambo wa chama chake cha Rwandan Movement for Democratic Change (MRCD).
Alikamatwa mnamo Agosti 2020 akiwa katika nchi ya Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) na kurudishwa nchini Rwanda kukabiliana na mashtaka ya ugaidi, utekaji nyara na mauaji.
Mwezi Julai mwaka 2018, FLN ilidai kuhusika na mashambulio katika mkoa wa kusini wa Rwanda.
Rusesabagina alifahamika kufuatia filamu ya Hotel Rwanda ikielezea jinsi alivyookoa maisha ya watutsi waliokuwa wamekimbilia katika hoteli moja mjini Kigali ambayo alikuwa ni meneja wake mwaka 1994.
Bwana Kagame amesema kwamba hajali kuhusu hadithi ya Bwana Rusesabagina kwamba yeye ni shujaa wa mauaji ya kimbari na kwamba ''hilo si jambo ambalo litakalomkabili mahakamani''.
"Kuna maswali ambayo lazima atayajibu...kuna wanaomsaidia wakiwa Ulaya, Marekani na kwingineko na ambao walimpandisha cheo na kumpa majina ya ushujaa, awe shujaa au laaah, mimi sina wasiwasi na hilo"-Rais Kagame.
Rais Paul Kagame amesema kikubwa sio ushujaa wa Bwana Rusesabagina au vitendo vyake wakati wa mauaji ya kimbari akisema kinachoangaliwa kwa sasa ni yeye.