Rais wa Uganda Yoweri Museveni, leo anaanza safari ya kutoka kijijini kwao akielekea mji wa Kampala ambapo atakuwa anasimama katika vituo kadhaa kwenye miji mbalimbali kutoa shukrani kwa wananchi.
Rais Museveni aliyeshinda tena uchaguzi wa urais wiki iliyopita ili kuongoza kwa muhula wa sita atasimama katika vituo saba akiwa njiani kurejea Kampala.
Msemaji wa serikali Ofwono Opondo ameandika taarifa za kina juu ya safari hiyo kwenye mtandao wa Twitter.
Safari hiyo ya Rais inawadia wakati wito umetolewa kwa serikali kuondoa kifungo cha nyumbani dhidi ya kiongozi wa upinzani Robert Kyagulanyi, maarufu kama Bobi Wine, ambaye anapinga matokeo ya uchaguzi.
Marekani imetoa wito wa kufanyika kwa uchunguzi katika madai ya wizi wa uchaguzi yaliyoibuliwa na upande wa upinzani ambao bado haujafanikiwa kuwasilisha ombi rasmi la kupinga matokeo.
Ofisi za upinzani zilivamiwa na jeshi na maafisa wa chama hicho wanasema nyenzo walizokuwa wanazikusanya kwa ajili ya kupinga matokeo ya uchaguzi walinyang’anywa na maafisa hao.