Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharif Hamad amezikwa nyumbani kwake katika kijiji cha Mtambwe Nyali mkoa wa Kaskazini Pemba.
Mwili wa Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad, uliagwa mapema leo asubuhi katika msikiti wa Maamur Upanga jijini Dar es Salaam kabla ya kupelekwa Zanzibar kwa ajili ya mazishi.
Viongozi mbalimbali wa kitaifa walishiriki ibada hiyo akiwemo Rais mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete na Kiongozi wa ACT-Wazalendo Zitto Kabwe.
Baadhi ya wananchi pamoja na viongozi waliohudhuria ibada ya mazishi ya Maalim Seif Sharif wamesema kuwa wamesikitishwa sana na msiba wa kiongozi huyo.
Mamia ya wazanzibari walijitokeza katika Viwanja vya Mnazi Mmoja vilivyopo mjini Unguja ambapo ndipo mwili ulipokelewa kutoka jijini Dar es Salaam kwa ajili ya dua kabla ya kusafirishwa kwenda kijijini kwake Mtambwe.