Mgombea wa urais nchini Uganda Robert Kyagulanyi, anayefahamika zaidi kama Bobi Wine ameahirisha kampeni zake.
Sababu za mgombea huyo wa urais kuahirisha kufanya kampeni zake ni kufuatia kujeruhiwa kwa maafisa wake wa kampeni na kuharibiwa kwa gari lake.
Kiongozi huyo wa upinzani anasema risasi zilifyatuliwa kwenye gari lake na kutoboa matairi ya gari lake na kumfanya asiweze kusafiri tena.
Video zilizosambazwa na timu yake ya kampeni kwenye mitandao ya kijamii zinaonesha kitu ambacho hakikutambuliwa kikilipuka umbali wa mita kadhaa kutoka mahali alipokuwa.
Awali katika eneo la Kayunga, mashariki mwa Kampala, gesi za kutoa machozi zilitumika kuwatawanya wafuasi wake.
Maafisa wanne wa kampeni yake walijeruhiwa Mmoja wao, aliyetambuliwa kama producer Dan Magic alipigwa usoni.
Mmoja wa polisi wanaowalinda wagombea wa urais waliotolewa na Tume ya Uchaguzi pia alijeruhiwa.
Takribani wiki mbili zilizopita, watu 54 waliuawa wakati wafuasi wa mgombea huyo walipokuwa wakiandamana kudai aachiliwe huru baada ya kukamatwa na polisi katika mkutano wa kampeni.