Serikali ya DRC yatangaza masharti mapya wakati wa mazishi nchini humo.
Hii ni kufuatia kuripotiwa kwa visa vya maambukizi ya corona nchini DRC, masharti mapya yametangazwa na serikali hasa kipindi cha mazishi ili kuepusha maambukizi zaidi.
Serikali ya nchini humo imetangaza kuwa watu wasiozidi ishirini ndio wataruhusiwa kuhudhuria mazishi, na atakayekiuka hatua hiyo atachukuliwa hatua za kisheria.
Wakati huohuo maafisa wa afya nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, wamesema watu 400 waliokuwa wameambukizwa virusi vya Corona wamepona.
Kwa mujibu wa maafisa hao, watu zaidi ya elfu Mbili na mia nane wameambukizwa virusi vya ugonjwa wa Covid-19, ambao umesababisha vifo vya watu 69.
Katika hatua nyingine, baadhi ya raia hawakupokea vizuri hatua ya serikali ambayo imetangaza utaratibu mpya wa mazishi hasa jijini Kinshasa huku waombolezaji wasiozidi 20 wakiruhusiwa kushiriki lengo likiwa ni kuepusha maambukizi zaidi.