Baada kufanikiwa kupata ushindi wa ugenini na nyumbani katika michezo miwili ya ligi ya mabingwa Africa baadhi ya wadau wa soka wameuomba uongozi wa klabu ya Simba kuendelea kumuamini kocha wao wa muda Juma Mgunda.
Wadau mbalimbali wa soka wameongea juu ya suala hili, akiwemo Mchezaji wa zamani wa timu ya Kariakoo ya Lindi na mchambuzi wa soka Jemedari Said amesema uongozi wa klabu ya Simba unatakiwa kuendelea kumuamini Mgunda kutokana na mabadiliko ya kiuchezaji aliyoyafanya kwenye timu hiyo. Mwenyekiti wa klabu ya Simba Murtaza Mangungu amesema wataendelea kuwa na kocha wao wa muda hadi pale uongozi wa klabu hiyo utakapotoa taarifa ya mabadiliko ya benchi la ufundi. Kocha wa muda wa klabu ya Simba Juma Mgunda ameiongoza timu hiyo katika michezo mitatu, mmoja wa ligi na miwili ya ligi ya mabingwa ambayo ameshinda michezo yote na kufunga mabao matano.