Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Amos Makalla amewaonya watendaji wanaowachia wafanyabiashara wadogowadogo maarufu machinga kurudi maeneo yaliyokatazwa.
Makalla ameonya juu ya hilo leo Jumatatu wakati akizindua mkakati wa usafi na uhifadhi mazingira wa mkoa huo uliopewa jina la "Safisha Pendezesha Dar es Salaam" baada ya kufanikisha kuwaondoa wafanyabiashara hao waliokuwa katika maeneo yasiyo rasmi.
Amesema watendaji wanapaswa kuelewa kuwa kuondolewa kwa wamachinga ni maagizo ya Rais hivyo kila mmoja ana wajibu wa kulisimamia hilo badala ya kuona ni kazi ya Mkuu wa Mkoa pekee.
"Nashukuru shughuli ya kuwaondoa wamachinga imeenda vizuri, kwani mpaka sasa tumefanikiwa kwa asilimia 90, sasa kuwaaacha warudi tena ina maana wewe mtendaji hujatimiza wajibu wako, hivyo hili sitalifumbia macho na ndio maana tumesainishana hadi mikataba hapa, tutaanzia hapo"-Amesema Makalla.
Makalla amezitaka taasisi ambazo wamachinga waliondolewa mbele ya majengo yao kuanza kuzilinda maeneo hayo wenyewe kwa kuwa kama mkoa wameshafanya kazi kubwa ya kuwasidia kuwaondoa.
Viongozi mbalimbali wa mkoa huo wakiwemo wakuu wa wilaya pamoja na baadhi ya wasanii wa muziki wa Bongo Fleva akiwemo Ali Kiba na Harmonize walishiriki katika uzinduzi wa mkakati wa usafi na uhifadhi mazingira wa mkoa wa Dar es Salaam.