Rais Samia suluhu Hassan leo Septemba 08, 2021 ametawazwa na Umoja wa Watemi wa Kisukuma kwa kushirikiana na Umoja wa Machifu nchini kuwa Chifu wa Machifu wote hapa nchini Tanzania.
Zoezi hilo limefanyika kwenye tamasha la utamaduni, Mila na Desturi katika viwanja vya Msalaba Mwekundu Kisesa wilayani Magu Mkoa wa Mwanza, Ambalo limeandaliwa na Umoja wa Machief Tanzania (UMT), Ambao wamemtawaza na kumpa jina la ‘Hangaya’ lenye maana ya ‘Nyota Inayong’aa’.
Katibu wa Umoja wa Machifu wa Kisukuma, Mtemi Aaroni Mikomangwa amesema jina hilo ni kutambua mchango wa Serikali anayoiongoza kwa kuthamini na kusimamia utu wa wanyonge pamoja na utamaduni wa Mtanzania.
“Tunaishukuru Serikali yako kwa kuthamini na kuenzi michango yetu Watanzania wote ikiwepo kuboresha sera za utamaduni kwa kushirikisha asasi za jadi nasi tu pamoja nawe katika kuinua utamaduni wa Taifa letu,”- Alisema Mikomangwa.
Aidha, ameiomba Serikali itambue rasmi machifu wa Tanzania kwa kuwapatia usajili rasmi wa umoja wao ili wawe kitu kimoja pamoja na kuwapatia machifu eneo mkoani Dodoma kwa ajili ya kuanzisha ofisi, miradi na kujenga makumbusho ya kitaifa.
“Pamoja na maombi yetu ya kutambuliwa, utekelezaji wa shughuli zetu unakabiliwa na changamoto ya kupoteza ya mazingira na udhibiti wa nyenzo tulizokuwa tukitumia kwa mfano kituo cha kichifu kilichopo maliya na nyumba zilizojengwa na machifu utemini jijini Mwanza,”-Aliongeza Mikomangwa
Rais Samia Suluhu Hassan amewasili jijini Mwanza kwa ajili ya kufunga tamasha la utamaduni wa Mtanzania linalofanyika katika viwanja vya Msalaba Mwekundu vilivyopo karibu na makumbusho ya Bujora wilayani Magu mkoani humo.
Tamasha hilo lilifunguliwa hapo jana Jumanne Septemba 7, 2021 na Naibu Waziri wa Ardhi, nyumba, Maendeleo ya Makazi lenye lengo la kudumisha, kurithisha na kuutangaza utamaduni wa makabila ya Tanzania limehitimishwa leo Septemba 08 baada ya Rais kutawazwa kuwa Chief wa Machief wote na limehudhuriwa na zaidi ya viongozi wa kimila kutoka makabila zaidi ya 120 ya Tanzania.