Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan amepokea chanjo dhidi ya Ugonjwa wa COVID-19, Ambayo ameizindua leo Julai 28, Katika Ikulu ya jijini Dar es Salaam.
Rais Samia ameizindua chanjo hiyo kwa kuwaongoza maafisa wengine wa serikali wakiwemo Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, Waziri wa Afya Dkt. Dorothy Gwajima, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Amosi Makala, Wakuu wa Wilaya mkoa huo pamoja na viongozi wa Dini na Madhehebu mbalimbali ambao walifika Ikulu kushiriki na Rais katika uzinduzi wa Chanjo hiyo ambao nao pia walipata fursa ya kuchanjwa.
Katika uzinduzi wa hafla ya chanjo chini humo rais Samia amesema serikali yake itahakikisha kwamba kila mtanzania nayetaka kuchanjwa anapata chanjo hiyo.
"Mimi ni mama ya watoto wanne,mimi ni bibi wa wajukuu kadhaa na pia mimi ni mke ..siwezi kujiweka katika hatari … Nimekubali kwa hiyari yangu na najua ndani ya mwili wangu nina chanjo kadhaa na nimeishi nazo kwa miaka karibu 61"- Alisema Rais Samia kabla ya kuchanjwa.
Aidha, katika hotuba yake wakati wa uzinduzi huo rais Samia amewataka wananchi kuendelea kuchukua tahadhari dhidi ya ugonjwa huo, Ambapo amesema kuna walioathiriwa na kuwapoteza jamaa zao ambao wangefurahia kuipata chanjo hiyo mapema.
"Kwa wale ambao familia zao hazijapitiwa na gonjwa hili ni vema wakaendelea kuchukua tahadhari na kujua umuhimu wa chanjo, Wakati gonjwa hili linapokugusa ndipo utajua hatari yake…nenda Moshi, nenda Kagera, nenda Arusha wana maneno ya kukuambia"- Alibainisha Rais Samia.
Rais Samia amesema kuna Watanzania ambao tayari walishachanjwa nje ya nchi ili kuendelea na shughuli zao za kibiashara na kikazi.
"Tunajua watu ambao wameshanjwa, wameeda kuchanja Afrika Kusini au Dubai.......na wanajua kama hawangechanjwa wangezuilika kufanya biashara zako hukona wala hawajaathirika na wanaendelea na biashara zao"-Rais Samia.
Rais Samia amesema Tanzania imeagiza dozi zaidi za chanjo ya Johnson and Johnson kupitia Umoja wa Afrika kama alivyoshauriwa na mkurugenzi wa Kituo cha Kudhibiti na kuzuia magonjwa barani Afrika (Africa CDC) Dkt. John Nkengasong, wakati alipofanya mazungumzo naye siku ya jumanne.