Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Gutterres amesema maeneo kadhaa katika jimbo la Tigray Kaskazini mwa Ethiopia yanakabiliwa na tisho la baa la njaa.
Gutterres ameonya, kwa kusema kuwa hali inaendelea kuwa mbaya zaidi endapo ufadhili hautaongezwa na njia za kufikia walioathiriwa haitaimarishwa.
''Hatua tunazochukua sasa zinaweza kuwaokoa watu wengi walio katika hatari ya kuangamia kutokana na ukosefu wa chakula"- alisema Gutterres.
Wakazi wa Magharibi mwa Tigray wameiambia BBC kwamba hawana chakula na kwamba wanakabiliwa na baa la njaa.
Watu wa wilaya ya Qafta Humera waliofikiwa kwa nji aya simu wamesema majambazi wamevamia mashamba yao na kuchukua mifugo yao.
Mark Lowcock ameiambia BBC kwamba mamia ya watu tayari wanakabiliwa na njaa katika eneo la Tigray kufuatia miezi kadhaa ya mapigano.
Mamlaka nchini Ethiopia inasisitiza kwamba hali ya utulivu imerejeshawa katika eneo hilo na njia za kuwafikia wakazi kufunguliwa.
Lakini UN inasema maelfu ya watu sasa wanaelekea kukabiliwa na baa la njaa kama lile lililoshuhudiwa mwaka 1984.
Mzozo ulizuka Tigray mwezi Novemba baada ya serikali ya Ethiopia kuanzisha oparesheni ya kijeshi ya kuondoa mamlakani chama tawala cha zamani TPLF, baada ya wapiganaji wake kuteka kambi za jeshi la muungano.