Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan, anatarajiwa kufanya ziara ya kikazi nchini Kenya Mei 04, 2021 siku ya Jumanne.
Rais Samia atakuwa katika ziara nchini humo kwa siku mbili ambapo atapokelewa na Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta.
Kupitia ziara hiyo, Rais Samia atafanya mazungumzo rasmi na mwenyeji wake Rais Kenyatta na kisha atalihutubia Bunge la Kenya litakalojumuisha Wabunge wa Mabunge yote mawili ya nchi hiyo.
Aidha, Rais Samiaa pia atahudhuria na kuhutubia mkutano wa jukwaa la wafanyabiashara wa Kenya na Tanzania utakaofanyika jijini Nairobi kwa lengo la kujadiliana masuala mbalimbali yahusuyo fursa za biashara na uwekezaji zilizopo Tanzania na Kenya.
Ziara hii ya nchini Kenya itakuwa ni safari ya pili kwa rais Samia Suluhu Hassan tangu alipoingia madarakani baada ya kifo cha Hayati Dkt John Pombe Magufuli.
Itakumbukwa kuwa Aprili 11, Rais Samia alifanya safari yake ya kwanza nchini Uganda na kukutana na Rais Yoweri Museveni akielezea kuwa lengo la ziara yake nchini humo ilikuwa ni kuimarisha uhusiano wa nchi mbili na kumaliza makubaliano ya mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi kutoka nchini Uganda.