Rais Samia Suluhu Hassan amepata ushindi wa asilimia mia moja ya wapiga kura wote katika chama cha CCM ambacho sehemu kubwa ya uongozi wake wa juu ni wanaume.
Wajumbe wapatao 1862 wa Chama cha Mapinduzi ambao ni sawa na asilimia 99 ya wajumbe wa chama hicho wamekutana leo Aprili 30, jijini Dodoma na rasmi wamemchagua Rais Samia Suluhu Hassan kuwa mwenyekiti wa CCM taifa.
Rais Samia anajaza nafasi hiyo baada ya kuachwa wazi na hayati John Pombe Magufuli ambae alifariki tarehe 17 mwezi Machi mwaka huu.
Hii itakuwa ni mara ya kwanza kwa wajumbe wa chama hicho tawala kukutana baada ya kifo Dkt. Magufuli lakini pia ni kikao cha kwanza kwa Samia kuhudhuria kama rais wa Tanzania, Ambapo hatua ya kihistoria katika chama hicho imeandikwa ya kuongozwa na mwanamke katika nafasi yake ya juu kabisa.
Wengi wanasubiri kwa hamu kuona ni mabadiliko gani atakayofanya mwenyekiti mpya baada ya kukabidhiwa mikoba ya kukuongoza Chama hicho kikongwe Afrika Mashariki kwa miaka mitano.
Mbali na kupigwa kura ya mwenyekiti, pia kumekuwa na upigaji kura ya wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa kutoka nafasi mbili ambazo zilikuwa wazi.
Halmashauri Kuu ya CCM pia imemteua mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Daniel Chongolo kuwa katibu mkuu wa chama hicho tawala kuchukua nafasi iliyoachwa wazi na Dkt. Bashiru Ally, Huku Shaka Hamidu Shaka ndiye aliyechaguliwa kuwa Katibu itikadi na uenezi mpya na kuchukua nafasi ya Humphrey Polepole.
Kikao hicho pia kimemteua Christina Mndeme kuwa Naibu Katibu Mkuu Bara huku Abdallah Juma Sadala akiendelea kuhudumu nafasi hiyo upande wa Zanzibar na katibu wa uchumi na fedha ni Frank Hawasi.