Watu wasiopungua 50 wameuawa mpaka sasa katika vita vilivyoanza Jumamosi iliyopita katika mji mkuu wa Darfur Magharibi na hofu bado imetanda kwa wakazi wa mji huo.
Vita hivyo viilianza kushuhudiwa siku nne zilizopita, katika mji wa El Geneina ambao ni mkuu wa Darfur Magharibi mwa Sudan na ulioko karibu kabisa na mpaka wa Chad.
Vita hivyo vimehusisha silaha ikiwemo risasi na makombora kwa mujibu wa wakaazi. Kamati ya madaktari wa eneo hilo imesema idadi walioikusanya mpaka hivi sasa ya waliouwawa ni watu 50 na waliojeruhiwa ni watu 132.
Kamati hiyo ya madaktari kupitia taarifa walioitowa wameeleza kwamba hali ya utulivu kiasi ilirejea jumatatu usiku lakini bado timu ya madaktari bado inahofia kuendelea na shughuli zake.
Shirika la uratibu wa msaada wa kibindamu la Umoja wa Mataifa OCHA jana liliripoti kwamba waliouwawa ni watu 40 na wengine 58 wamejeruhiwa katika machafuko hayo ya kikabila kati ya jamii ya wenye asili ya kiarabu na wale wasiokuwa wa asili ya kiarabu wa kabila la Massalit.
Hii leo mkazi mmoja kwa jina Mohammed Abdel-Rahman-wa El-Geneina kunakotokea mapigano hayo amezungumza na shirika la habari la AFP kwa njia ya simu na kusema kwamba hali ya utulivu ilikuwepo usiku lakini leo asubuhi walisikia milio ya risasi kutoka upande wa wilaya ya Hay Al-Jabal ambayo ilidumu kwa takriban saa nzima.
Umoja wa Mataifa umetangaza kuzuia safari zake za ndege na shughuli zake zote za msaada katika mji unaokabiliwa na machafuko ambao ni kituo kikuu cha shughuli za msaada wa kihutu.
Sio mara ya kwanza machafuko kushuhudiwa katika mji huo,yamewahi kutokea mapigano mnamo mwezi Januari mwaka huu wakati watu wa jamii ya kabila la Masalit kumuua mtu kutoka jamii ya asili ya kiarabu.