Rais John Magufuli amezindua barabara ya juu eneo la Ubungo ambayo imepewa jina la Marehemu John Kijazi, ambaye alikuwa Katibu Mkuu Kiongozi pamoja na kituo cha kimataifa cha mabasi cha Mbezi Luis.
Katika uzinduzi huo Rais Magufuli amewaonya wakandarasi wanaochelewesha miradi ya serikali kwa kusingizia janga la corona.
Barabara hiyo ambayo ni ya kwanza kushuhudiwa nchini inatazamwa kama ni kiunganishi muhimu kwa wakazi wa jiji la Dar es Salaam na mikoa mingine inayotumia kiunganishi hicho kufanya safari za ndani ya Dar es Salaam, pamoja na kwenda nchi jirani.
Akizungumza kwenye uzinduzi wa barabara hiyo iliyoko kwenye maunganiko ya Barabara ya Sam Nujoma na Ubungo, Rais Magufuli amesema kukamilika kwake kunaandika historia mpya ya jiji la Dar es Salaam ambalo limepata kuwa makao makuu ya nchi kwa zaidi ya miaka 60.
Amesema daraja hilo siyo tu kwamba limeondoa adha na kero ya muda mrefu ya foleni, lakini pia linatoa picha halisi kuwa Dar es Salaam ni jiji la kibiashara.
"Ni laazima Dar es Salaam liwe jiji kweli la kisasa, ni lazima ibaki kuwa paliwahi kuwa makao makuu ya serikali yetu."-Rais Magufuli.
Kukamilika kwa ujenzi wa daraja hili ni sehemu tu ya hatua nyingine zinazoendelea kuchukuliwa na serikali na uboreshaji wa miundombinu ya barabara na madaraja ya juu na hivi sasa mradi mwingine wa ujenzi wa barabara ya njia nane unaendelea kutekelezwa katika eneo la Pwani.
Kwa kiasi kikubwa miradi hiyo inaendelea kulifanya jiji la Dar es Salaam kuwa la aina yake.
Hata hivyo, Rais Magufuli ametumia fursa hiyo kuwaonya wakandarasi wanaofanya shughuli zao kwa kusuasasua akisema siku zao sasa zinahesabika.
Mbali ya kuzinduliwa kwa barabara hiyo, Rais Magufuli pia amezindua kitua kipya cha kisasa cha mabasi yaendayo mikoani na nchi jirani.
Kituo hicho kilichojengwa eneo la Kimara nje kidogo ya katikati ya jiji, kinajumuisha pia maeneo ya wafanyabiashara ndogondogo na wale wakubwa.
Mradi wa barabara ya juu uliopewa jina la Kijazi Interchange unakamilika ukiwa ulipatiwa fedha za mkopo wenye masharti nafuu kutoka Benki ya Dunia wenye thamani ya zaidi ya shilingi Bilioni 200, ukichangiwa na fedha za serikali.Huku ujenzi wa kituo cha mabasi cha Mbezi Luis ukitumia kiasi cha zaidi ya Shilingi Bilioni 50.