Mazishi ya Katibu Mkuu Kiongozi Mhandisi Balozi John Kijazi yamefanyika katika mji wa Korogwe Tanga.
Mwili wa balozi huyo ulifikishwa katika eneo maalum lililoandaliwa kwa ajili ya ibada maalum ya mazishi ya kumuaga kabla ya mazishi.
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa pamoja na viongozi wengine wa Serikali wameshiriki katika ibada hiyo pamoja na familia na pia walifika katika makaburini kwa ajili ya maziko.
Itakumbukwa kuwa Februari 19, Rais wa Tanzania John Magufuli aliongoza waombolezaji katika kuaga mwili wa Katibu Mkuu Kiongozi John Kijazi katika viwanja vya Karimjee jijini Dar es salaam.
Kwa mujibu wa taarifa ya Kurugenzi ya mawasiliano Ikulu, Balozi Kijazi alifariki katika hospitali ya Benjamin Mkapa jijini Dodoma alipokuwa akipatiwa matibabu.
Balozi Mhandisi John William Herbert Kijazi amekuwa mwakilishi wa Tanzania nchini India, Singapore, Sri Lanka, Bangladesh na Nepal mwenye makazi yake jijini New Delhi, India kuanzia mwaka 2007 - 2016 na hivyo kumfanya kuwa Mkuu wa Mabalozi wote wanaowakilisha Tanzania nje ya nchi.