Taifa la Rwanda limesema linasubiri kupata ufafanuzi kuhusu sababu ya Uingereza kuchukua hatua ya kuiwekea marufuku ya wageni wanaosafiri au kupitia nchini Rwanda kuingia Uingereza.
Hii ni baada ya Uingereza kutangaza kuweka marufuku dhidi ya wasafiri wanaotoka Rwanda, Burundi na Umoja wa falme za kiarabu kuingia nchini Uingereza wiki hii.
Katika taarifa yake iliyotumwa kwenye mitandao ya kijamii, serikali ya Rwanda imesema kuwa, Rwanda imeweza kushughulikia vyema udhibiti wa maambukizi ya Covid -19, ikiwa ni pamoja na kupima, kufuatilia waliokutana na wenye maambukizi, kuwadhibiti wenye maambukizi, kutibu na taarifa kuhusu zake kuhusu virusi vya corona zimekuwa za wazi na kuthibitishwa na taasisi huru.
Taarifa hiyo imeendelea kusema kuwa Rwanda ni moja ya nchi chache ambazo zinazingatia kupimwa kwa Covid 19 kwa wasafiri wote wanaoondoka na wale wote wanaopitia nchini humo kuelekea nchi nyingine.
Rwanda inasema ukizingatia orodha ya nchi za kikanda ambazo zimeathiriwa na ambazo haziojaathiriwa na marufuku, taarifa chache zilizotolewa Rwanda hazina uchunguzi wa kisayansi.
Aidha, Rwanda imeikumbusha Uingereza kuwa haikujiunga na marufuku zilizowekwa na mataifa mengine za wasafiri kutoka Uingereza mwaka 2020 kutokana aina mpya ya virusi vya corona vilivyogundulika katika baadhi ya maeneo ya Uingereza.
Rwanda na Burundi zinajiunga na Tanzania, Jamuhuri ya Kidemokrasia ya Congo na Afrika Kusini ambazo pia zimewekewa marufuku hiyo na Uingereza.
Kulingana na taarifa iliyotolewa na Uingereza, hatua hiyo inalenga kudhibiti kuenea kwa aina mpya ya kirusi cha Afrika Kusini, na marufuku hiyo inaanza kufanya kazi siku ya Ijumaa saa saba kwa saa za Uingereza.
Raia wa Uingereza, Ireland na raia wenye haki ya makazi nchini Uingereza wataruhusiwa kuingia, lakini kwa sharti la kujitenga kwa siku 10 wakiwa nyumbani.
Pia safari za moja kwa moja za ndege za abiria kutoka Uingereza kwenda Umoja wa falme za kiarabu zitapigwa marufuku.
Waziri wa usafiri Grant Shapps alisema abiria wanaoruhusiwa kuingia Uingereza watahitaji uthibitisho kuwa hawana maambukizi ya virusi vya corona kabla ya kuwasili, vinginevyo watapigwa faini ya pauni 500.
Chanzo na BBC Swahili.