Mateka mwingine nchini Mali, mwanamke wa Uswisi, ameuawa na watekaji nyara waliokuwa wakimshikilia.
Mamlaka ya Uswisi hatangaza jina la mateka huyo ambaye anadaiwa kuuawa, mwandishi wetu huko Geneva, Jérémie Lanche, ameripoti.
Mmisionari huyo mwenye umri wa miaka 40 ambaye alizaliwa Basel, alitekwa nyara miaka minne iliyopita huko Timbuktu na kundi lenye mafungamano na al-Qaeda.
Aliwahi kutekwa nyara kwa muda mfupi mwaka 2012, wakati mji huo ulianguka mikononi mwa wanajihadi, Na alionekana kwenye video ya watekaji nyara mwaka 2017, huku akionekana kuwa ni mdhaifu na amekonda.
Mmisionari huyo aliuawa mwezi mmoja uliyopita, Sophie Pétronin, mateka wa Ufaransa aliyeachiliwa hivi karibuni nchini Mali, ambaye aliwasili nchini Ufaransa jana Ijumaa ndiye alitoa taarifa kuhusu kifo chake kwa mamlaka nchini Ufaransa.
Waziri wa mambo ya Nje wa Uswisi, Ignazio Cassis, amelaani kile alichokiita "kitendo cha kikatili" na ametoa "rambi rambi kwa familia ya marehemu".
Duru za kuaminika zinabaini kwamba mmisionari huyo "aliuawa na watekaji nyara wa kundi la kigaidi la Kiislamu la Jama'at Nasr al-Islam wal Muslim".
Uswisi sasa inatafuta kujua mazingira halisi ya kifo cha raia wake, na pia wapi ulipo mwili wake.