Rais wa Marekani Donald Trump amesema kwamba yeye na mke wake Melania Trump wamepatikana na virusi vya corona na wako karantini.
Rais Trump ametoa taarifa hiyo kupitia mtandao wa Twitter.
Tangazo hilo linawadia baada ya Bwana Trump na wasaidizi wake wawili kuthibitishwa kuambukizwa virusi vya corona.
Aidha, awali mke wa rais Melania Trump alituma ujumbe kuashiria kwamba wanaendelea vizuri ambapo aliandika; ''Kama ambavyo raia wengi wa Marekani wamefanya mwaka huu, Rais Trump na mimi tuko kwenye karantini nyumbani baada ya kuthibitishwa kuwa na virusi vya corona.Tunaendelea vizuri na nimeahirisha shughuli zote zijazo.Tafadhali hakikisha uko salama na tutashinda changamoto hii pamoja.''
Hope Hicks, 31, ambaye ni mshauri wa rais amekuwa msaidizi wa karibu wa Bwana Trump kupatikana na virusi vya corona hadi hivi sasa.
Bi. Hicks alisafiri na Bwana Trump kwa ndege ya kijeshi kwenda kwenye mdahalo wa Televisheni alipokabiliana na mpinzani wake Joe Biden Jumanne.
Mapema Alhamisi, Bwana Trump alisema yeye na mke wake Melania wanakwenda karantini baada ya Bi. Hicks kuthibitishwa kuwa na corona.
Bado haijafahamika wala kuthibitishwa kama kugundulika huko kwa Rais Trump kutaathiri maandalizi ya mdahalo wa pili wa urais, ambao umepangwa kufanyika Oktoba 15 huko Miami, Florida.