Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Angellah Kairuki amesema Serikali imetoa Shilingi bilioni 13.88 kwa ajili ya kuboresha huduma za afya katika Mkoa wa Kigoma.
Kairuki ameyabainisha hayo katika ziara ya Rais Samia Suluhu Hassan kuzungumza na wananchi wa Mkoa wa Kigoma kwenye Uwanja wa Lake Tanganyika.
Amesema kati ya fedha hizo zilizotolewa kwa mwaka 2021/22, Sh bilioni 6.6 zimetumika katika ujenzi na ukamilishaji wa vituo vya afya 15 na bilioni 1.2 zimeelekezwa kwenye ukamilishaji wa ujenzi wa Zahanati 24 katika Mkoa wa Kigoma.
Aidha pia amebainisha kuwa Sh bilioni 3.5 zilitolewa kwa ajili ya ujenzi wa hospitali katika halmashauri 6 za Buhigwe, Kakonko, Kasulu DC, Kigoma DC, Kigoma MC na Uvinza DC.
Kuhusu miundombinu ya barabara, Kairuki amesema, Serikali imetoa Sh bilioni 21.7 kwa ajili ya kuimarisha barabara na imepanga kuitumia bilioni 34.1 kwa ajili ya kutekeleza Mradi wa Uboreshaji Miji (TACTIC) ambao umelenga kuboresha miundombinu katika Manispaa ya Kigoma Ujiji.