Rais wa Tanzania, Samia Suluhu ametoa sababu ya kwanini taasisi za dini zinazotoa huduma katika sekta za afya na elimu zinatozwa na serikali, Ambapo amesema kuwa ni kwasababu baadhi zinafanya biashara na si kutoa huduma kama ilivyozoeleka.
Rais Samia amesema hayo kupitia mkutano mkuu wa 31 wa Jumuiya ya Kikristo Tanzania CCT alioufungua ambao umedfanyika mkoani Morogoro.
Rais amebainisha kuwa wakati mwingine taasisi za dini hujenga shule au hospitali katika eneo ambali serikali imekwishajenga kituo cha afya.
“Hapa ndipo panapokuja lile suala linalolalamikiwa la ushindani wa huduma, taasisi ya dini ina hospitali yake hapo Serikali inajenga kituo cha afya hapo kwa kuona wananchi wakienda huku wanatoa pesa nyingi zaidi kuliko wakipata huduma serikalini”-Amesema Rais Samia.
Rais Samia amesema lengo la Serikali ni kupunguza ugumu wa maisha kwa wananchi ambapo suluhisho lake ni kufanya kazi kwa uwazi na kuaminiana ili wanaotoza kodi wajue taasisi za dini hazifanyi kazi kibiashara.
“Hapa utaona wale wamekusanya jasho la watu wengine sisi tunaenda kutoza kodi, haya yote ni kwa sababu hatukuwa na uwazi, niombe sasa tufanye kazi kwa uwazi na kuaminiana”-Ameeleza Rais.
Katika upande mwingine Rais amevunja ukimya wa sababu ya bei ya mafuta kupanda nchini akisema ni mkakati wa Serikali kuongeza fedha kwa Wakala wa Barabara Mijini na Vijijini (TARURA) ili kuimarisha ujenzi wa barabara hizo.
“Nataka niwape taarifa kwamba tumeongeza fedha kidogo kwenye mafuta. Pengine mmesikia kelele za mafuta, lakini tumeongeza Sh100 katika kila lita ya mafuta ili tuweze kukusanya fedha zikatusaidie kujenga barabara za vijijini”- amesema Rais Samia.
Aidha Rais amefafanua kuwa fedha nyingi zimepotea katika ujenzi na ukarabati wa barabara ambazo zimekuwa zikiharibiwa na mvua.