Rais Samia Suluhu Hassan amesema serikali itaendelea kufanya kazi kwa kushirikiana na vyombo vya habari, ambapo amevitaka vyombo hivyo kuendelea kufuata kanuni na taratibu zilizowekwa.
Rais Samia amebainisha hayo wakati akizungumza na Wahariri wa Vyombo mbalimbali vya Habari jijini Dar es Salaam.
"Kwa ujumla kama tunavyofahamu vyombo vya habari mbali ya kutoa taarifa kwa umma vina mchango mkubwa kulinda umoja wa kitaifa,..... usalama wa nchi na kuchochea shughuli za maendeleo pia vinasaidia sana kufichua maovu kwenye jamii"- Rais Samia
Katika upande mwingine kuhusu suala la Corona Rais Samia amesema serikali itafanya chanjo ya hiyari ili kwenda sambamba na Dunia inavyokwenda.
“Nilipoingia madarakani nilitamani tushughulike na hili jambo kama linavyoshughulikiwa ulimwenguni, na kwahiyo nikataka kujua ukubwa wake na tunalo hili janga kiasi gani, nikaunda kamati ya waataalam.........nilishasema nitakaa na wenzangu Wanasiasa tuone tunakwenda na siasa zetu katika mustakabali mpana wa Taifa, Nchi yetu ina vitu vingi, Corona inatupiga, uchumi umeshuka tunaupandisha nimesema nakwenda kuifungua Nchi naomba nipeni muda halafu tutakwenda kwenye mengine”—Rais Samia
Rais Samia Suluhu Hassan ameshiriki mahojiano na Wahariri wa Vyombo vya Habari mbalimbali kuhusu siku 100 tangu kuingia kwake madarakani, ambayo yamefanyika ikulu jijini Dar es Salaam.