Chama cha ACT Wazalendo kimewafahamisha wanachama wake, pamoja na umma wa Watanzania kuwa Mwenyekiti wake Maalim Sei Sharif Hamad na mkewe Bi Awena, wamethibitika kupata maambukizi ya Covid 19.
Kulingana na taarifa ya chama iliyotumwa kwenye mitandao yake ya kijamii, ACT Wazalendo imesema kuwa wasaidizi kadhaa wa Makamu huyo wa Rais wa Zanzibar pia wamepatikana na virusi vya corona baada ya kufanyiwa vipimo.
''Katika hali ya kuchukua tahadhari zaidi madaktari walimshauri Maalim Seif kuwa ni vyema awepo chini ya uangalizi maalum katika kipindi chote atakachokuwa anaendelea na matibabu'', imesema taarifa ya ACT iliyotumwa kwenye ukurasa rasmi wa Twitter wa chama.
Kulingana na taarifa hiyo Maalim Seif amepumzishwa katika Hospitali ya Mzazi Mmoja, Unguja, ambako anaendelea kuwa chini ya uangalizi wa karibu wa madaktari.