Mwalimu mmoja wa shule ya msingi ya Gitega nchini Burundi yuko mikononi mwa polisi kwa shutuma za kuwatesa watoto wa shule anaowafundisha.
Mwalimu Espeye Nzeyimana Ecofo Ngobeke, ambaye ni mwalimu wa somo la Kifaransa darasa la nne anasemekana aliwaadhibu wanafunzi 30 kwa kushindwa kujibu maswali aliyowauliza.
Watoto 30 kati ya 45 ni wanafunzi wake waliofeli na akaamua kuwapa adhabu ya kuzunguka uwanja uliojaa mawe kwa magoti.
Magoti yao yalianza kuchubuka na kutokwa damu na ikabidi wapelekwe wote hospitalini kutibiwa.
Afisa elimu katika eneo la Mubuga ilipo shule ya Ngobeke Manirambona Placide, anasema mwalimu huyo yuko mikononi mwa polisi.
"Nzeyimana Esperee alisimamishwa kazi Jumapili asubuhi, na kupelekwa mjini Gitega ambako anasubiri kufikishwa mahakamani"- Alisema Bw. Manirambona Placide.
Taarifa zilizotolewa na polisi zinasema kuwa baada ya kuona jinsi wanafunzi wake walivyoumia, mwalimu huyo hakuonekana tena kazini.
ChanzoBBCSwahili