Idadi isiyofahamika ya mamba wadogo hawajulikani walipo baada ya kutoroka katika shamba wanapofugwa eneo la Cape Magharibi Afrika Kusini Jumatano, kulingana na vyombo vya habari vya eneo hilo.
Juhudi za kutafuta mamba hao kila mmoja akiwa na urefu wa zaidi ya mita moja zinaendelea.
Aidha, inashukiwa kwamba huenda wamepata njia inayowapeleka kwenye mto Breede ulio karibu.
"Ni hatari kiasi fulani kwa jamii kwasababu wamekuwa wakifungwa na wamezoea chakula cha kawaida, hawajitafutii chakula".
Msemaji wa serikali eneo hilo James-Brent Styan pia amenukuliwa na gazeti la Times Live akisema kuwa wanyama hao ni hatari kama wengine wowote wale wa aina hiyo ambao ni hatari kwa binadamu.
Takribani mamba 20 wamerejeshwa katika shamba wanapofugwa, kulingana na afisa wa eneo aliyenukuliwa na Tovuti ya Eye Witness News.
Chanzo: BBC Swahili