Bilionea Saniniu Laizer kutoka Mirerani mkoani Manyara, ambaye wiki kadhaa zilizopita mnamo mwezi Juni alipata Madini yenye uzito mkubwa zaidi kuwahi kutokea ambayo aliyauza kwa serikali na kuingia kwenye orodha ya mabilionea wapya wa Tanzania nyota yake imeendelea kung'aa.
Hatimaye Bilionea huyo leo ameuza jiwe lingine la Tanzanite kwa Serikali lenye kilo 6.3 na kukabidhiwa mfano wa hundi ya shillingi Bilioni 4.8.
Katika makabidhiano hayo yaliyofanyika leo Agosti 03 Mirerani baadhi ya viongozi wa serikali waliweza kuhudhuria hafla hiyo ili kushuhudia makabidhiano hayo akiwemo Waziri wa Madini Dotto Biteko na Waziri wa Fedha Dkt. Philip Mpango.
Kwa upande wake Bilionea Laizer ametoa wito wa kutokukata tamaa kwa wafanyabiashara na wachimbaji wengine wadogo wa madini, Ambapo amesema yeye binafsi alianza kuwa mfanyabiashara mdogo wa madini kwa miaka 10 na hajawahi kukata tamaa;
“Mimi nawashauri wachimbaji wadogo wasikate tamaa, mimi imenichukua miaka 10 katika shughuli hizi, nao ipo siku watafanikiwa”- Saniniu Laizer
Saniniu Kuryan Laizer mwenye umri wa miaka 52, ni mume wa wanawake wanne na amejaliwa watoto 30.