Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Freeman Mbowe tayari amechukua fomu ya kuwania nafasi ya Urais katika Uchaguzi Mkuu utakaofanyika mwezi Oktoba 2020.
Licha ya Mwenyekiti huyo kuchukua fomu leo, Chama hicho pia leo Juni 17, 2020, kimetangaza majina ya Wanachama wake wengine walioomba kuteuliwa na Chama hicho kugombea nafasi ya Urais katika Uchaguzi Mkuu mwezi Oktoba.
Majina hayo yametajwa leo ambapo imesisitizwa kuwa mchakato wa awali ulikuwa unahusisha kuandika barua ya kutia nia na sio kuchukua na kurudisha fomu, hivyo watu walioandika barua kwa Katibu Mkuu John Mnyika ni 11.
Wanachama wengine waliokuwa wameshachukua fomu za kuwania kiti cha urais ni pamoja na Tundu Lissu na Peter Msigwa,Lazaro Nyalandu, Mwita Isaya, Dkt Majinge Mayrose, Manyama Leonard, Nicodemus Gasper, Nalo Opio, Neo Richmond na Shaaban Msafiri.
Aidha taarifa hiyo imefafanua kuwa kuna baadhi ya wanachama ambao wameelezwa kuwa ni bodaboda walijikusanya na kumwandikia barua mtu mmoja (ambaye hajatajwa) ili agombee lakini barua yao haikukidhi vigezo kutonana na kuwepo kwa sharti la mtu mwenyewe kuandika barua na sio kuandikiwa.