Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii,Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu amezindua kituo cha huduma za simu kwa wateja.
Kituo hicho ambacho kimezinduliwa leo kazi yake kubwa itakuwa ni kutoa elimu sahihi kwa jamii kuhusu masuala mbalimbali ya Afya yakiwemo magonjwa ya milipuko.
Kituo hicho kina uwezo wa kupokea simu 1000 kwa watu mmoja na kuunganisha vituo vitano kwa wakati mmoja.
Waziri Ummy ameelezea kazi ya kituo hicho kuwa ni kupokea maoni, taarifa, maswali na ushauri kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu sekta ya afya na amewataka wananchi kupiga simu 199 ili wapate huduma hiyo na walioko nje ya nchi wanapaswa kupiga namba.0800110124.
Katika uzinduzi huo Waziri Ummy ametoa rai kwa watakaopiga simu kuwa wastaarabu, kutumia lugha ya staha, na kutoa taarifa sahihi ambazo zitaisaidia serikali na Wizara ya Afya kuchukua hatua stahiki na kwa wakati.
Kituo hicho kilichozinduliwa leo kitakuwa na wataalamu 150 wakiwemo wa afya, Wauguzi na Madaktari.
Amependekeza kituo hicho kipewe jina la “Afya Call Centre’ badala ya jina la “Kituo cha Huduma za Simu” ambacho kitakuwa kikishughulikia magonjwa yote.
Waziri Ummy amesema endapo Wizara ya Afya itaweza kutumia vizuri Tehama, itatatua changamoto mbalimbali zilizoko kwenye Sekta hiyo, Huku akiitaka Jamii itambue kinga ni bora kuliko tiba.