Mkuu wa mkoa wa Mara Adam Malima ameviagiza vyombo vya Dola kuwakamata wazazi wanaohatarisha maisha ya watoto wao dhidi ya maambukizi ya corona kwa kuwatuma kununua mahitaji sokoni au maeneo yenye mikusanyiko ya watu.
Hatua hiyo ya mkuu wa mkoa huu wa Mara Adam Malima inatokana na uwepo wa idadi kubwa ya watoto wadogo katika mikusanyiko ya watu wazima ilihali hakuna tahadhari yeyote iliyochukuliwa na wazazi pamoja na jamii juu yao.
Malima ametoa agizo hilo wakati alipokuwa akizungumza na wafanyabiashara katika soko kuu la mji wa Bunda huku akionya kuwa iwapo suala hilo litaendelea atalifunga soko hilo na kuwaondoa watu wote wasifanye biashara.
Awali wakielezea hatua walizozichukua kukabiliana na tatizo la ugonjwa huu hata hususani la watu kukataa kunawa mikono pindi waingiapo sokoni viongozi wa eneo hilo wamesema nguvu za ziada zinahitajika ili watu kunawa mikono pindi wanapoingia ndani ya soko hilo.
Kwa upande wao wafanyabiashara katika soko hilo wakizungumzia suala hilo wamesema wamajipanga vyema kuhakikisha kila mteja anafuata maelekezo ya serikali.
Mkoa wa Mara unatajwa kuwa na watu wenye tabia za ukorofi, wanaopenda kukataa kutii maagizo na maelekezo ya serikali kwa visingizio mbalimbali hatua inayotajwa huenda ikasababisha kuenea Zaidi kwa maambukizi ya virusi vya corona.