Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli ametoa ahadi ya kuwaajiri madaktari 1000 katika vituo vya afya pamoja na hospitali zilizopo nchini.
Rais Magufuli ametoa kauli hiyo wakati akisikiliza changamoto za Madaktari katika ukumbi wa JINCC Dar es Salaam kwenye ufunguzi wa kongamano la kitaaluma la chama cha madaktari Tanzania.
Rais Magufuli ametoa ahadi hiyo baada ya Naibu Waziri wa Afya Dkt. Faustine Ndugulile pamoja na Rais wa Chama cha Madaktari Tanzania M.A.T Dkt. Elisha Osati kuelezea changamoto ya upungufu wa rasilimali watu iliyopo katika hospitali pamoja na vituo vya afya vilivyopo nchini.
Amesema madaktari watakaoajiriwa ni wale ambao wamekaa kwa miaka mitano bila kazi na pia ameitaka wizara ya afya kuwasaidia madaktari wanaoanzisha taasisi zao binafsi kwa ajili ya kutoa huduma za afya na kuwasihi madaktari wengine kujitahidi kuwa wabunifu walau kutengeneza dawa za kusukutua meno, kutengeza dawa za fungus hata kwa kuanzisha viwanda vidogovidogo ambayo itasaidia kupunguza uagizwaji wa dawa kutoka nje ya nchi.
Katika upande mwingine Rais Magufuli amewataka viongozi wa siasa kuacha kuwatishia madaktari pindi mgonjwa anapopoteza maisha na badala yake sheria ifuate mkondo wake, pamoja na hayo amewasihi madaktari kuwa na hulka ya kuonyana wao kwa wao kabla ya wanasiasa kuwaweka kituo cha polisi kwamasaa 48 kwasababu ya mgonjwa kupoteza maisha.
Madaktari hao 1000 watakaoajiriwa wanatarajiwa kufanya kazi katika vituo vya afya Zaidi ya 300 pamoja na hospitali za wilaya zaidi ya 70 zilizopo nchini.
Chama Cha Madaktari Tanzania M.A.T kimefikisha miaka 55 mwaka huu tangu kuanzishwa kwake ambacho kinajumuisha madaktari kutoka hospitali za umma na hospitali binafsi
Mwisho.