Rais wa jamhuri ya muungano wa Tanzania Dkt. John Magufuli amemuagiza waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Suleiman Jaffo kumfukuza kazi mtumishi wa halmashauri ya wilaya ya kilosa Daniel Elimringi kwa kosa la kuchana kitabu kitakatifu cha dini ya kiislam,qur’ani.
Taarifa na Piensia Rugarabamu
Rais Magufuli ametoa agizo hilo wakati akizungumza na wakazi wa Kigamboni mara baada ya kuzindua wilaya mpya ya kigamboni iliyoambatana na uzinduzi wa jengo la utawala la mkuu wa wilaya hiyo ambapo amesema licha ya Waziri Jafo kumsimamisha kazi mtumishi huyo, serikali haiwezi kufanya kazi na watumishi wa namna hiyo.
Katika hatua nyingine rais Magufuli ameiagiza Wizara ya Ardhi kuhakikisha zaidi ya hekari 750 za ardhi iliyokuwa shamba la nafco napco zilizoko chini ya wizara ya ardhi zinarejeshwa kwa manispaa ya Kigamboni ndani ya wiki mbili.
Akifafanua kuhusu jengo hilo mkuu wa wilaya ya kigamboni Sarah Msafiri amesema litasaidia wakazi wa wilaya hiyo kupata huduma kwa urahisi huku akibainisha kupungua kwa matukio ya uhalifu katika wilaya hiyo na kuhaidi kumalizika kwa utekelezwaji wa mradi wa umeme hivi karibuni.
Viongozi mbalimbali waliohudhuria uzinduzi huo wamebainisha changamoto zilizopo katika wilaya hiyo.
Hata hivyo Rais Magufuli ameendelea kutoa onyo kwa wananchi wanaoishi mabondeni konte nchini kuzingatia agizo la waziri mkuu kuondoka maeneo hayo na kwamba serikali haitojihusisha kugharamia athari za mafuriko kwa wote wanaokaidi agizo hilo.
Mwisho.