Mamlaka ya kuthibiti na kupambana na dawa za kulevya nchini imemkamata mwekezaji raia wa Poland Damian Sanikowsiki (40) kwa tuhuma za kuzalisha na kumiliki shamba la bangi, Kata ya Njia Panda Mashariki eneo la Mji mdogo wa Himo Wilaya ya Moshi.
Taarifa na Rodrick Mushi
Kaimu Kamishna Jeneral wa mamlaka ya kuthibiti na kupambana na dawa za kulevya nchini james Kaji amesema wamefanikiwa kumkamata mwekezaji huyo baada ya kupata taarifa kutoka kwa raia wema juu ya kilimo cha mazao ya bangi kilichokuwa kikiendelea kwenye eneo hilo ambalo limezungushiwa ukuta.
Kaimu Kamishna amesema kuwa mara baada ya kikosi kazi kufika katika eneo hilo mwekezaji alishawishi kutoa rushwa ya Tsh milioni 10 huku akiwaahidi kuendelea kuwapatia kiasi cha Tsh milioni 40 kila mwezi kwa ajili ya kumaliza suala hilo.
Kwa upande wake mwekezaji aliyekamatwa amesema amekuwa akifanya uzalishaji wa bangi na kwa ajili ya wateja wake wakubwa waliopo ndani na nje nchi..
Uongozi wa mtaa umesema mwekezaji huyo alinunua eneo hilo kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha watoto yatima na uwekezaji wa hoteli eneo ambalo ameligeuza kwa ajili ya kilimo haramu cha bangi.
Mwisho