Mamlaka ya wanyamapori wilayani Serengeti imelazimika kumuua kwa risasi mnyama aina ya chui baada juhudi za kumrejesha kwenye hifadhi kugonga mwamba ambapo inadaiwa chui huyo alivamia makazi ya watu katika Kijiji cha Bisarara mapema siku ya Jumanne na kusababisha madhara ikiwemo kuua mifugo na kujeruhi watu sita.
Ilikuwa ni hali ya sintofahamu kwa wakazi wa Kijiji cha Bisarara wilayani Serengeti ambayo iliwagubika mara baada ya mnyama chui kuingia kijijini kwao na ambapo mnyama huyo aliua mifugo yao na kujeruhi wakazi sita wa kijiji hicho.
Wakazi hao wamesema wanyama hao wamekuwa shida kwenye makazi yao na wameiomba serikali kuweza kulitazama suala hili pindi wanyama wakali wanapofika katika makazi ya watu.
“Mnyama akifa inakuwa ni shida lakini binadamu akijeruhiwa hatua zinachelewa kuchukuliwa hivyo tunaiomba serikali iweze kuchukua hatua mapema kuweza kunusuru maisha yetu’- Gasper Magesa-Mwananchi
Afisa wa wanyama pori Deokali Mtaita amekiri kuwepo kwa mnyama huyo na amesema mara baada ya kupata taarifa ya kuwepo kwa mnyama huyo katika Kijiji cha Bisarara walichukua hatua ya kwenda kumrudisha hifadhini lakini juhudi zao ziligonga mwamba ndipo waakaamua kumpiga risasi kwa lengo la kuwaokoa wakazi wa Kijiji hicho.
Wakati huohuo mtendaji wa kijiji cha Bisarara Mang’era Magesa ameilalamikia idara ya wanyamapori kutofika eneo la tukio kwa wakati, hali ambayo imechangia kuwasababisha wananchi majeraha pamoja na kuharibifu mali zao.
“Hawa wanyama mara kwa mara wanatusumbua hii ni mara ya tatu na sio hao tu, kuna unyayo umepatikana asubuhi yule chui aliyeuwa ni dume, chui jike bado hajapatikana mimi natoa wito kwa serikali iwasaidie watu hawa waliojeruhiwa angalau waweze kupata huduma ya matibabu”;Mang’era Magesa - Mtendaji Wa Kijiji Cha Bisarara.
Wanyama wakali katika wilaya ya Serengeti wamekuwa wakivamia makazi ya watu wanoishi ndani ya vijiji vilivyopo pembezoni na hifadhi na wamekuwa wakileta hofu kwa wakazi wa hapo hali inayowasabia kuishi maisha ya sintofahamu juu ya kesho yao.
Mwisho.