Taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa (TAKUKURU), mkoa wa Simiyu imewakamata na kuwafikisha mahakamani watendaji watatu wa serikali kwa nyakati tofauti, na hakimu wa mahakama ya mwanzo kwa tuhuma za kuomba na kupokea rushwa.
Akizungumza na waandishi wa habari mkuu wa TAKUKURU mkoa wa Simiyu bwana Edili Elinipenda amesema watendaji hao wamekamatwa na kufikishwa mahakamani na kufunguliwa mashitaka ya kuomba na kupokea rushwa kinyume cha sheria.
Elinipenda amemtaja afisa mtendaji kata ya Bunamhala Kalimbiya Gambuna ambaye anakabiliwa na mashitaka manne tofauti yaliyofunguliwa mahakama ya mkoa wa Simiyu baada ya kuwakamata wazazi wa wanafunzi watoro na kuwaweka mahabusu ya kata kisha kuwatoa baada ya kupokea rushwa.
Nae mtendaji wa Mwamapalala Anthony Peter anashikiliwa kwa kosa la kuomba na kupokea rushwa shilingi 200,000 kutoka kwa mkandarasi anayejenga barabara ya kiwango cha lami Maswa na Bariadi ili asichukuliwe hatua baada ya kulipua miamba kwa kutumia baruti katika muda ambao ni kinyume na makubaliano. Afisa mtendaji wa kata ya Ikindilo Sita Masunga kuwa anakabiliwa na tuhuma ya kuomba na kupokea rushwa ya shilingi elf 80,000 ili amwachie mtuhumiwa ambaye alikuwa mahabusu ya kata kwa siku nne bila kupelekwa mahakamani. Vilevile amemtaja hakimu wa mahakama ya mwanzo Nyakabindi Liberatha Mhagama anayekabiliwa na kosa la kuomba na kupokea rushwa ya shilingi elfu, 80,000 ili aandike hati ya kumtoa mahabusu mshitakiwa aliyekuwa gerezani ambaye kesi yake ilikuwa inasikilizwa na hakimu huyo.