MAUAJI YA KUKATA MAKOROMEO:Washtakiwa wahukumiwa kunyongwa hadi kufa
Mahakama kuu kanda ya Bukoba imewahukumu kunyongwa hadi kufa watu Watatu kwa kuhusika na mauaji ya wakazi wanne wa kata ya Katoma wilaya ya Bukoba Mkoani Kagera mwaka 2015.
Washtakiwa hao Watatu Aliyuu Dauda ,Rashid Athuman na Ngesela Keya wametiwa hatiani baada ya kuhusishwa na Mauaji ya mfululizo yaliyokuwa yakitokea kuanzia mwezi Januari hadi Novemba mwaka 2015 maarufu kama mauaji ya Makoromeo kutokana na watu waliokuwa wakikutwa wameuawa
Washtakiwa katika kesi hiyo namba 66 ya mwaka 2017 wamedaiwa kutekeleza mauaji ya Marehemu Vedasto John ,Anastella Paschal ,Emmanuel Joseph na Evodius Aloys kwa siku tofauti katika mwezi Oktoba Mwaka 2015 katika kata ya Katoma wilaya ya Bukoba Vijijini.
Jaji Mfawidhi Lameck Mlacha akisoma hukumu hiyo amesema hukumu hiyo imezingatia ushahidi wa kimazingira,kukiri pamoja na baadhi ya vitu walivyokutwa navyo washtakiwa ambavyo vilitumika kutekeleza mauaji hayo.
Akisoma hukumu iliyochukua takribani saa mbili na nusu Jaji Mlacha amesema hakuna ushahidi unaoonyesha watuhumiwa hao wakitekeleza mauaji hayo moja kwa moja lakini ushahidi wa kimazingira umebaini kuwepo kwa mawasiliano ya karibu ya washtakiwa wote Watatu .
Aidha Jaji Mlacha amesema mkanda wa CD umeonyesha washtakiwa hao wakikiri mbele ya viongozi wa eneo husika na polisi kuwa walidhamiria kufanya mauaji hayo kutokana na imani za kidini huku vipimo vya DNA vikionyesha kuwepo na uhusiano kati ya sime na mapanga vilivyotumika katika mauaji baina ya Washtakiwa na baadhi ya sehemu za miili ya marehemu hao kama nywele na kucha. Kadhalika namba ya simu ya mmoja wa marehemu hao ilipatikana ikiwa imewekewa namba za mshtakiwa wa pili ambaye ni Rashid Athuman ambaye aliitumia kuwasiliana na washtakiwa wenzake mara kwa mara kuhusiana na mipango yao ya kutekeleza mauaji zaidi.
Aidha washtakiwa hao walikutwa wakiwa na baadhi ya nyaraka za makanisa mbalimbali Kumi na Matatu yaliyochomwa moto kwa nyakati tofauti mwaka 2015. Upande wa Jamhuri katika kesi hiyo umeongozwa na wakili Mkuu wa serikali Hashim Ngole ilhali upande wa utetezi ukiongozwa na Mathias Rweyemamu ambaye amesema jopo lake linatarajia kuandaa hoja za kukata rufaa kwa watuhumiwa hao ambao Mnamo Mwezi April mwaka huu walihukumiwa kifungo cha maisha jela baada ya kupatikana na hatia ya Kuchoma makanisa kumi na matatu katika wilaya za Missenyi,Bukoba na Muleba