NEC imesema inatumia fedha za ndani katika zoezi la maboresho ya Daftari la kudumu la wapiga kura ili kuifanya Tume hiyo kuwa huru na kuwajibika bila kuingiliwa na wahisani katika mipango na mchakato wa uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020.
Wakati Tanzania ikitarajiwa kuingia katika uchaguzi wa serikali za mitaa mwaka huu na Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani mwaka 2020, Tume ya Taifa ya Uchaguzi ipo katika maandalizi ya uboreshaji wa Daftari la wapiga kura zoezi ambalo litaanza Julai mwaka huu. Dkt. Athumani Kihamia Mkurugenzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi ametolea
ufafanuzi wa wapiga kura watakaokutwa na zoezi la uchaguzi wakiwa eneo tofauti na walipojiandikisha na kwamba Tume hiyo ipo tayari kuwaruhusu kupiga kura kama kutafanyika marekebisho ya sheria ya sasa ya uchaguzi. Hata hivyo suala la ushiriki wa watu wenye ulemavu bado limeonekana kutotiliwa mkazo huku walemavu wakilalamikia miundombinu isiyo rafiki inayowanyima haki ya kupiga kura. Maamuzi yoyote katika mchakato wa uchaguzi mara nyingi huwagusa kwa kiasi kikubwa wanawake ambao mara nyingi hujiandikisha kwa wingi na kupiga kura tofauti na wanaume. Tume ya Taifa ya Uchaguzi imeendelea kukutana na wadau mbalimbali na kutoa elimu juu ya zoezi la uboreshaji wa daftari la wapiga kura ambapo imekutana na Asasi za wanawake, Walemavu na Vijana.