Hospitali ya wilaya ya Nyamagana mkoani Mwanza inayohudumia kati ya wagonjwa 200 hadi 500 kwa siku na kutoa huduma mbalimbali za matibabu imeomba wadau kujitokeza kwa wingi kusaidia kufanya usafi wa mazingira na kukusanya taka zinazozalishwa katika hospitali hiyo ili kuepukana na magonjwa ya mlipuko.
Christopher Juma ni kaimu mganga mfawidhi wa hospitali ya wilaya ya Nyamgana mkoani Mwanza ametoa Rai hiyo baada ya Umoja wa wapiga debe na makondakta jiji la Mwanza kufanya usafi katika maeneo mbalimbali ya hospitali hiyo. Kaimu mganga huyo amesema kitendo ambacho kimefanywa na umoja wa wapiga debe na makondakta wa mkoa wa Mwanza cha kujitolea kufanya usafi katika baadhi ya mawodi za wagonjwa kimeleta faraja si kwa uongozi wa hospitali bali hata kwa wagonjwa.
Katibu wa vijana wa CCM mkoa wa Mwanza UVCCM Mariam Amiri ambaye ni mlezi wa umoja huo akiongoza umoja wa wapiga debe na makondakta mkoa wa Mwanza kufanya usafi ikiwemo kufyeka na kuzoa taka na katika baadhi ya wodi amesema ni kwa kiasi gani wanavyoonesha kama wanathamini suala la usafi.
Baadhi ya wagonjwa ambao wamelazwa katika hospitali hiyo wamepongeza hatua iliyofikiwa na umoja wa wapigadebe mkoa wa Mwanza ya kufanya usafi na kuomba wadau wengine waige mfano kama huo. Wapiga debe na makondakta wameahidi kuendelea na jitihada za kufanya usafi katika maeneo mbalimbali hasa yenye uhitaji ili kukabiliana na uchafuzi wa mazingira kwa lengo la kuepukana na magonjwa ya mlipuko.
Picha na mtandao.