Mahakama kuu kanda ya Musoma mkoani Mara imepokea kesi zaidi ya mia mbili zikiwemo mpya hamsini ambazo zimefunguliwa na wananchi waliokuwa wamekosa fursa ya kwenda mahakama kuu ya kanda ya ziwa iliyopo jijini Mwanza kutokana na kutokuwa na fedha na gharama za kujikimu.
Kwa miaka zaidi ya 50 sasa mkoa wa Mara ulikuwa hauna huduma ya mahakama kuu hatua iliyokuwa ikisababisha wananchi wengi kushindwa kutafuta haki zao kwa kukosa nauli na gharama za kwenda mahakama kuu kanda ya ziwa jijini Mwanza.
Ikiwa ni siku ya kwanza kukabidhiwa ofisi za utendaji majaji wawili na msajiri mahakama kuu kanda ya Musoma,zaidi ya kesi mia mbili zimepokelewa na watendaji hao ili kuanza kushughulikiwa.
Wakizungumzia kuanza kwa majukumu yao ya kikazi katika mahakama hiyo Jaji mfawidhi wa mahakama ya kanda ya Musoma Ndugu, John Kayoza na jaji Zephrine Galeba wanasema kuwa wapo tayari kutoa haki katika mashauri mbali mbali.
Nae kaimu mkuu wa mkoa Dkt; Vicenty Naano na katibu tawala wa mkoa wa Mara Bi; Carolina Mthapula wakizungumzia ujio wa mahakama hiyo wanawataka wananchi wote kuhakikisha wanapeleka mashauri yao ili yaweze kupatiwa haki.
Mahakama kuu kanda ya Musoma imeanza kazi rasmi mkoani Mara huku ikianza kushughulika na mashauri yote yaliyopo katika mahakama kuu kanda ya mwanza yaliyokuwa yamefunguliwa na wananchi wa mkoa huu na kuweza kuyamaliza ifikapo mwezi wa saba mwaka huu.