Wafanyabiashara wa soko kuu la mjini Njombe wameiomba halmashauri ya mji kuwasamehe kodi kwa muda ili kuwawezesha kurejesha gharama walizopoteza wakati wa kuhama kwenye soko hilo kupisha ujenzi wa soko jipya.
Wakizungumza na Startv wafanya biashara hao wamesema kuwa wamelazimika kuiomba halmashauri kuwasamehe kodi kwa muda ili waweze kurejesha gharama za mitaji yao walizotumia katika harakati za kupisha ujenzi wa soko hilo.
Katika hatua nyingine wafanyabiashara hao wamepiga ndulu za kuitaka halmashauri kurekebisha miundombinu ya soko walilopelekwa kwa sasa kwani usalama wa mali zao umekuwa ni mdogo kutokana na kukosekana kwa huduma za muhimu kama umeme na barabara.
Star tv imemtafuta mwenyekiti wa halmashauri ya mji wa njombe Edwin Mwanzinga ambae amekubali kuwasamehe wafanyabiashara hao kodi kwa muda huku akiahidi kulifikisha katika vikao vya baraza suala hilo ili kutatua changamoto zinazowakabili katika soko hilo walilopelekwa kwa sasa.
Takribani mwaka mmoja umepita tangu kuwepo kwa malumbano baina ya wafanyabiashara wa soko kuu la mjini Njombe kuhusu kuondolewa ili kupisha ujenzi wa soko jipya ambapo hatimaye hadi kufikia sasa wafanyabiashara hao wamekubali kung’oka kwa hiari licha ya kupoteza gharama nyingi walizowekeza.
Picha na mtandao.