Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhandisi Hamad Masauni ameliagiza Jeshi la Polisi Nchini na Baraza la Taifa na Usalama barabarani kuhakikisha wanayakamata mabasi yote yasiyo na vidhibiti mwendo.
Masauni ametoa agizo hilo wakati akizindua baraza la Taifa la Usalama Barabarani makao makuu ya Nchi Dodoma ambapo, amesema miongoni mwa vyanzo vya ajali Nchini ni mwendo kasi unaosababishwa na madereva wazembe wasiofuata sheria za usalama barabarani kitendo kinachopelekea ajali nyingi.
Kwa upande wake Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Jamanne Sagini ambaye Pia ni Mwenyekiti wa Balaza la Taifa la Usalama barabarani amesema baraza hilo kwa kushirikiana na baraza la kazi litaendelea kutoa mafunzo ya Usalama barabarani kwa viongozi wa umma wakiwemo makatibu wakuu na wabunge ili kuwajengea uwezo wa kukemea matukio ambayo yanayosababisha ajali kutokea.
Aidha Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza Kamishna Msaidizi mwandamizi wa Polisi SACP. Wilbroad Mutafugwa amesema kuwa Baraza la Taifa la Usalama Barabarani tangu limeanzishwa kusimamia kamati za Mikoa na Wilaya limesaidia kusimamia matumizi sahihi ya fedha zilizotokana na ada za ukaguzi wa magari mbalimbali.