Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchini IGP. Camilius Wambura ameunda tume huru kuchunguza tukio la mauaji ya watu wawili waliouawa baada ya askari kutumia mabomu ya machozi na risasi za moto katika vurugu zilitokea Kijiji cha Ikwambi Kata Mofu Wilaya ya Kilombero Mkoani Morogoro.
IGP. amesema tume hiyo itakuwa chini ya Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai wa Jeshi la Polisi ambapo itachunguza chanzo cha tukio hilo na kutambua endapo kulikuwa na sababu za kutumia risasi za moto katika kukabili vurugu zilizokuwepo zilizohusisha wafugaji ambao walikamatwa na kuwafungia viongozi kadhaa wa Kijiji hicho.
Tukio hilo lilitokea jana Oktoba 23, 2022 na kwa mujibu wa Mkuu wa mkoa wa Morogoro Fatma Mwasa amesema chanzo ni wakulima ambao ni wakazi wa kijiji hicho kuwafungia ndani ya ofisi ya Kijiji wenyeviti wa vitongoji, vijiji pamoja na Wafugaji kwa lengo la kutaka kuwachoma Moto wakiwatuhumu kushindwa kuwasaidia pindi wafugaji wanapoingiza mifugo katika mashamba yao.
Miongoni mwa waliojeruhiwa ni Diwani wa kata hiyo Greyson Mgonela, ambaye baada ya kufanya mazungumzo naye kwa njia ya simu amesema wakati vurugu zinatokea wananchi walikuwa wakitumia silaha za jadi, Mawe, Mikuki na Marungu kuwapiga Askari, huku Askari nao wakitumia Mabomu ya Machozi na Kisha Risasi za Moto.