Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ametoa wito kwa Wakandarasi na Taasisi nyingine za sekta binafsi kuzingatia weledi, maadili na uaminifu katika majukumu yao ili wanapotekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo iweze kuleta tija kwenye maisha ya Watanzania.
Amesema Serikali inatambua mchango wa sekta binafsi katika kuleta maendeleo na kukuza uchumi nchini. “Sekta binafsi imechangia kwa kiasi kikubwa ukuaji katika sekta mbalimbali ikiwemo elimu, viwanda sanaa, mawasiliano pamoja na utalii”.
Waziri Mkuu ameyasema hayo leo (Jumamosi, Desemba 11, 2021) alipofungua mkutano wa 21 wa Wanachama wa TPSF na kongamano la biashara na uwekezaji, katika ukumbi wa maktaba mpya ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam Mkoani Dar es Salaam.
Waziri Mkuu amesema Serikali itaendelea kuishirikisha sekta binafsi katika ziara za Serikali nje ya nchi kama alivyofanya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwenye ziara za nchi za Kenya, Burundi, Marekani, Malawi, Msumbiji na Uganda.
“Nitumie fursa hii kuwashukuru kwa mchango mkubwa katika kukuza uchumi wa Tanzania kupitia utengenezaji wa ajira, kukuza kipato cha wananchi, kutengeneza bidhaa, kuongeza pato la Taifa na kuongeza uwezo wa nchi kujitegemea, endeleeni kushiriki katika ujenzi wa miradi mbalimbali ya kimkakati, pamoja na kuhakikisha mnawekeza katika maeneo ya vijijini ”
Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amesema Serikali imeendelea kuondoa na kupunguza kodi, ushuru na tozo mbalimbali zilizokuwa kero kwa wafanyabiashara na wawekezaji kupitia Sheria za Fedha kwa vipindi tofauti.